Jumamosi, 13 Desemba 2014

CAG akague Bodi ya Sukari- Waziri Chiza



 

Dar es Salaam, Serikali imemwagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali kukagua Bodi ya Sukari ili kubaini kama kuna aliyehusika kutoa kibali cha kuagiza sukari kutoka nje kwa mwaka 2013/14.
Kauli ya Serikali imekuja siku chache baada ya Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) Zitto Kabwe kusema kuwa ataanza kulifanyia kazi sakata la sukari nchini.
Zitto alisema PAC italifanyia kazi suala hilo kwa sababu ya malalamiko ya wamiliki wa viwanda vya sukari yanayotolewa kutokana na soko la ndani kutekwa na sukari inayoingizwa kutoka nje ya nchi na wafanyabiashara wakubwa.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Mhandisi Christopher Chiza alisema kuwa kazi ya kutoa kibali siyo ya waziri wala katibu mkuu bali ni ya Bodi ya Sukari hivyo kuna haja ya kufanyika ukaguzi na ikibainika kuna waliohusika wawajibishwe.
Serikali haijashindwa kupambana na wahalifu wanaoagiza sukari ya magendo, na ndiyo maana mwaka 2013/14 hakuna kibali cha kuruhusu kuagiza sukari nje ya nchi kilichotolewa cha kushangaza imejaa sokoni ina maana kuna hila imefanyika ambayo inatakiwa ibainishwe na mkaguzi mkuu.
“Atakayebainika ametoa kibali cha kuruhusu kuingiza sukari mwaka 2013/14 atawajibishwa kwa sababu taarifa zilizopo hakuna kilichotolewa na sukari imefurika sokoni, ”alisema Waziri Chiza.
Chiza alisema mahitaji ya sukari kwa mwaka ni tani 590, 000, viwanda vya ndani huzalisha tani 300,000, sukari inayoagizwa kwa ajili ya viwanda ni tani 170,000, hivyo mahitaji yanayobaki huagizwa nje ya nchi kwa vibali kutoka Bodi ya Sukari.
Chiza alisema kuwa siyo sukari tu, bali bidhaa nyingine zinaingizwa kwa magendo wengine wakitumia Bandari ya Zanzibar.
Alifafanua kuwa hiyo sukari ya magendo pia inatakiwa kuchunguzwa ubora wake kwa kuwa wengine wanatumia sukari ya viwandani kwa matumizi ya ndani , lazima wakaguzi wakague ubora na viwango vya sukari hiyo.
“Serikali haijashindwa kupambana na wanaoingiza sukari ya magendo, kama ambavyo vita dhidi ya dawa za kulevya inavyofanikiwa basi na hili linawezekana,” alisema Waziri Chiza.
Alisema mkakati mwingine ni kukata kodi sukari inayoagizwa kwa ajili ya viwanda na kuanzisha mfumo mmoja wa kutoza kodi mizigo unaosimamiwa na Mamlaka ya Mapato (TRA).
Kuhusu malalamiko ya wamiliki wa viwanda vya sukari nchini Chiza alisema kuwa walishakubaliana kungana kuagiza sukari pamoja.

0 maoni:

Chapisha Maoni