Jumapili, 1 Juni 2014

Mizengo Pinda ataka kanuni za Bunge zibadilishwe

 
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda  

Dodoma. Uamuzi wa wabunge wa Kambi Rasmi ya Upinzani kutoka nje ya Ukumbi wa Bunge wakisusia uhitimishaji wa mjadala wa Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini, kimemzindua Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye amependekeza kubadilishwa kwa kanuni za Bunge ili kuwadhibiti.
Pinda alitoa kauli hiyo juzi usiku baada ya bajeti hiyo iliyogomewa na wapinzani kupitishwa na wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) pekee, huku akisisitiza kuwa tabia hiyo ifike wakati ikomeshwe.
Wabunge hao wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), waliamua kususia mjadala huo kwa madai ya kutoridhishwa na ulivyokuwa ukiendeshwa kwa mikakati waliyowekeana wabunge wa CCM ya kufukia kashfa nzito ya IPTL inayoikabili wizara hiyo.
Kiongozi wa Kambi hiyo, Freeman Mbowe alisema amefuatilia mjadala huo, lakini kwa bahati mbaya umegubikwa na ukinzani wa kiitikadi na makundi, kwamba wabunge wanajadili kwa kujaribu kufukia mambo mazito kwa sababu ya mitazamo ya makundi na kiitikadi, hivyo siyo busara kuendelea kushiriki.
Katika maelezo yake, Pinda alisema: “Inawezekana kanuni zinaruhusu, lakini haiwezekani kila mnaposhindwa hoja muone njia rahisi ni kutoka nje, nasema hivi ili Watanzania waone kuwa hali hii siyo nzuri.”
Alisema hoja zikitolewa wapinzani wanatakiwa kukaa na kuzisikiliza na kwamba jibu siyo kutoka nje bali ni kushindana hadi hatua ya mwisho.
“Tabia inaendelea kujengeka na siyo nzuri. Tuombe kanuni za Bunge zirekebishwe kwa sababu Bunge linaonekana halina watu wakati hao waliotoka hawana sababu za msingi” alisema Pinda.
Pinda aliiponda taarifa ya upinzani iliyosomwa na Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika kwamba haikuwa na jambo la msingi na ilijaa maneno mengi.
“Mnyika ameongea maneno mengi, sikuona jambo la msingi, angalau angechagua mambo mawili makubwa na kuyazungumza ili tumsikie” alisema.
Akizungumzia sakata la IPTL, Pinda alisema jambo hilo sasa linachunguzwa na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuwataka wabunge kutolijadili mpaka hapo ukweli utakapowekwa wazi.
Pinda alisema ili kuhakikisha huduma za umeme na maji zinawafikia wananchi, amemwagiza Waziri wa Fedha kufumba macho kutafuta fedha ikibidi hata kukata fedha za posho ili ziende katika miradi ya maji na umeme.
“Kutokana na umuhimu wa baadhi ya sekta, nililazimika kutoa maelekezo kwa Waziri wa Fedha. Ikiwezekana hata tukatwe posho zote za miezi miwili maana hatuwezi kufa. Posho hizo ziende kusaidia huko vijijini. Hili ni suala la kufa na kupona watu hawana umeme na maji”, alisema Pinda.

0 maoni:

Chapisha Maoni