Jumanne, 10 Juni 2014

Nauli za Daladala jijini Dar kupanda hadi sh. 800, Wanafunzi nao kuumia.....Eneo moja kwenda jingine ni dakika 30 tu



Hatimaye picha halisi ya gharama ya Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka Dar es Salaam (Dart) awamu ya kwanza, imeonesha nauli ya basi kutoka maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam kwenda na kurudi vituo vikubwa vikiwemo vya Kariakoo na Posta, itapanda kutoka nauli ya chini ya Sh 400 ya sasa mpaka Sh 700 na Sh 800 kwa ruti moja. 

 

Kwa wanafunzi, nauli kwa ruti moja kwenda katika vituo hivyo vikubwa katika mradi huo ambao utaanza kwa majaribio mwishoni mwa mwaka huu, zitapanda kutoka Sh 200 mpaka nusu ya nauli ya mtu mzima kwa ruti husika.

 
Aidha, mfumo wa uendeshaji wa mradi huo na nauli, umewekwa katika sehemu mbili; sehemu ya kwanza ni usafirishaji wa abiria kutoka maeneo ya ndani ya makazi ya watu mpaka katika vituo vidogo na vikubwa vilivyopo barabara kuu za Dart, za Morogoro na Kawawa kwa sasa na sehemu ya pili ni usafirishaji wa abiria kutoka katika vituo vilivyopo katika barabara kuu ya Dart za Morogoro na Kawawa, kwenda vituo vikuu vikiwemo Kariakoo na Posta.
 
Hayo yamebainishwa jana jijini Dar es Salaam, katika taarifa ya mwisho ya Makubaliano ya Dart, iliyotolewa katika mkutano wa Mashauriano ya Uwekezaji wa awamu ya kwanza ya mradi huo wa Dart.
 
Taarifa hiyo imebainisha kuwa, abiria atakayelazimika kusafiri na mabasi ya Dart kwa safari fupi ndani ya barabara zilizo katika makazi ya watu, kwa mfano wa barabara inayopita Sinza; kutoka Bamaga mpaka Shekilango, atalipa Sh 500, tofauti na sasa ambapo analipa Sh 400.
 
Kwa atakayetumia mabasi ya Dart kutoka katika barabara ndogo zilizopo katika makazi ya watu, kwenda katika vituo vikubwa vya Dart vilivyopo njia kuu za Morogoro na Kawawa ili kwenda Kariakoo, Posta au Kimara, atalazimika kukata tiketi ya Sh 800, atakayoitumia kupata usafiri kutoka barabara ndogo na katika barabara kubwa.
 
Mfano wa nauli hiyo, ni abiria anayetoka maeneo hayo ya Sinza kwenda Kimara, Kariakoo au Posta, ambaye atalazimika kukata tiketi ya Sh 800, itakayomwezesha kupakia basi la Dart kutoka maeneo hayo mpaka Shekilango, ambako atabadilisha basi kwa tiketi hiyo hiyo, kwenda Kariakoo, Posta au Kimara. 
 
Aidha kwa abiria watakaolazimika kutumia mabasi matatu ya Dart, kutoka katika barabara ndogo zilizopo katika makazi ya watu, kupitia barabara kuu za Dart na kwenda katika eneo lililopo katika barabara ndogo za makazi ya watu, watalazimika kulipa Sh 900 kwa mabasi yote matatu.
 
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mabasi yatakayotumika kubeba abiria kwenye njia kuu, yatachukua watu zaidi ya 150 kwa basi moja, ambapo abiria watakaopata viti vya kuketi ni 52 na wengine wamewekewa eneo nadhifu la kusimama.
 
Kwa mabasi yatakayobeba abiria kutoka njia ndogo zilizopo katika makazi ya watu, yatachukua watu zaidi ya 80, kati ya hao abiria 42 ndio watakaopata nafasi ya kukaa na waliobakia wamewekewa nafasi nadhifu ya kusimama.
 
Kuhusu muda utakaotumika kwenye ruti moja ya mabasi hayo ya Dart, abiria atatumia muda wa dakika zisizozidi 30 kufika anakokwenda, akitumia mabasi kwenye njia kuu, tofauti na sasa ambapo kwa kutumia daladala abiria hutumia zaidi ya saa mbili kufika waendako. 
 
Akizungumza katika mkutano huo, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Jumanne Sagini, utaratibu wa ulipaji nauli kwenye mabasi ya Dart, utakuwa ni wa kutumia mfumo wa kadi ambapo abiria anatakiwa anunue tiketi kabla ya safari.
 
 “Hakuna kulipa nauli ndani ya basi, abiria anatakiwa alipe kabla ya kuanza safari, na kama unapanda mabasi matatu, unatakiwa kulipa nauli yote kwa mara moja kisha unapewa tiketi, unapoingia kwenye basi msomaji atachukua tiketi yako na kuipitisha kwenye mashine na kupunguza nauli ya safari hiyo, hadi hatua ya mwisho wa safari,” alisema Sagini.
 
Alisema utaratibu huo, utapunguza au kuondoa kero kwa abiria na  katika mabasi madogo yanayobeba abiria kuwaunganisha kwenye njia kuu,  yatakuwa na vifaa vya mawasiliano baina ya dereva aliye barabara ndogo na dereva aliye barabara kuu za Dart.
 
Kwa mujibu wa Sagini, mradi huo ukianza, abiria watanunua tiketi kwa kupitia huduma za fedha kwa njia ya simu kama vile M-pesa, Tigo-pesa, Pesa Fasta na Airtel Money. 
 
Alisema ili kuzuia wizi na udanganyifu kwenye vituo vya mauzo ya tiketi na kwenye vituo vya mabasi, zinafungwa kamera na video ili kuimarisha ulinzi, na kuhakikisha mapato halali kwa ruti zinazofanywa.
 
“Hii itasaidia kuondoa wizi na uhujumu unaoweza kufanywa katika vituo vya abiria,” alisema Sagini.
 
Alisema kwa hatua hiyo, dalaldala za sasa zitaondolewa katika zaidi ya njia 43 ambazo ziko kwenye barabara ya Morogoro na barabara ya Kawawa na katika ruti nyingine, daladala hizo zitaendelea kuondolewa hadi hapo ujenzi wa barabara zote za Dart utakapokamilika.
 
Katika mabasi hayo ya kubeba abiria kwenye njia kuu za Dart, mabasi yanayoruhusiwa ni yale yatakayokidhi vigezo, ambavyo ni pamoja na kuwa na upana wa meta 18 na uwezo wa kubeba abiria 150, ambayo yanahitajika mabasi 145.
 
Kwa mabasi yatakayosogeza abiria hadi njia kuu, yatatakiwa yawe na uwezo wa kubeba abiria zaidi ya 80 na upana wa meta 12 na yatatakiwa mabasi 90.
 
Akitoa mwito kwa wawekezaji wa ndani na nje, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia, alisema ni vyema katika sekta binafsi, wadau wa usafiri na watu mbalimbali wachangamkie fursa hiyo.
 
Alisema Serikali kupitia mfumo wa ushirikishaji sekta binafsi, umeona ni vyema kushirikisha wadau hao kwenye mradi huo mkubwa Afrika Mashariki, ambao ukitumika vizuri ni chachu ya maendeleo na ukuaji uchumi.

0 maoni:

Chapisha Maoni